BOMOA BOMOA KUANZA APRILI 12 DAR ES SALAAM

0

0:00

HABARI KUU

Mratibu wa Miradi ya Ushirikiano Kati ya Benki ya Dunia na Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), Mhandisi Humphrey Kanyenye amesema Ofisi ya Uratibu wa Mradi wa Bonde la Msimbazi, kwa kushirikiana na ofisi za wakurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam na Manispaa ya Kinondoni, itaanza kubomoa nyumba zilizofidiwa Aprili 12, 2024.

Ni kwa muktadha huo, wananchi wote ambao wamekwishalipwa fidia wanatakiwa kuondoka katika maeneo yao kabla ya tarehe hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 25, 2024 jijini Dar es Salaam, Kanyenye amesema kwa mujibu wa makubaliano wote ambao wameshapokea malipo yao wanatakiwa kuhamisha mali zao na kupisha eneo la mradi ndani ya wiki sita baada ya kupokea fedha hizo kwenye akaunti zao.

Amesema kuwa muda huo umeshakamilika kwa idadi kubwa ya waliolipwa ambapo mpaka kufikia Machi 21, 2024, tayari waathirika 2,155 wa zoezi hilo kati ya 2,329 walikuwa wamelipwa kiasi cha shilingi bilioni 52.6.

Ameongeza kuwa awamu hii ya utekelezaji wa zoezi hili itawahusisha wale ambao wamefikisha wiki sita zilizotolewa baada ya kupokea malipo ya fidia hadi kufikia tarehe Februari 29, 2024.

Pia amesema kuwa, daftari la pili fidia la waathirika 446 ambao hawakufikiwa katika uthamini wa awali kwa sababu mbalimbali limeshakamilika na litawasilishwa kwa Mthamini Mkuu wa Serikali kwa ajili ya kusainiwa Machi 26, 2024 tayari kwa kulipwa fidia.

Mujuni Henry
Author: Mujuni Henry

JUNIITV


Discover more from JUNIITV.ONLINE

Subscribe to get the latest posts sent to your email.

Don't miss out!
Invalid email address

Leave a Reply

Discover more from JUNIITV.ONLINE

Subscribe now to keep reading and get access to the full archive.

Continue reading